KUNI MBICHI!



                                                    
Kuni mbichi ni msaliti wa moto. Torati zake ni kuufilisisha moto halafu kumshawishi chakula asihusiane na binadamu. Majipu yalikuwa yameshauteka mwili wangu nyara pasi huruma yoyote. Japo nilijizatiti niyakwaruze kwa, maji nayo yalikuwa yashamwagika na bila shaka kiu iliyonigubika ilizidi kuninyonga hata karibu nigeuke mwehu. Maisha nayo yalikuwa yametukodolea macho utadhani ibilisi alikuwa akiyaongoza. Chakula nacho kilikuwa nadra ja maji jangwani. Kuparara kwetu nako kulikuwa jambo jingine la kuzungumzia kwani macho yatakulipuka kwa mshangao ndugu. Miili yetu ilikuwa imebaki mifupa hata ladha ya kuwa binadamu ikawa shubiri. Kweli dunia si gunia la kuchezea ndugu na asiye na mwana atazame uhondo wa mchafuko wa kimazingira ya kibin-mateso dhidi ya sanamu wa kibin-adamu. Maisha nayo ni mshikomshiko na ukishikwa nawe shikamana na hiyo ni tahadhari kwako. Tumbo langu je? Lim’baki upara ambao umechuchumaa kwa undani kana kwamba laomboleza kifo cha shibe.
Jamani mbona mimi na wenzangu tuteteseke hivi ilhali wengine wasaza hadi vyakula vyatupiliwa mbwa vile? Kumbuka tunaye rafiki aliyetuhutubia kwa wak’ti mmoja akiomba msaada wetu. Kwani ni msaada gani bwana Micah we? Aah! Ulikuwa msaada mdogo jamani wa kimakaratasi tu. Yaani KURA shoga! Kwa kweli hilo lilikuwa jambo dogo sana lisilohitaji hata hotuba yoyote kuliomba. Baada ya kupewa mapeni ambayo yaliisha kwa kitumbo usiku huo tuliweza kushawishika kiubongo na tukampa zote bila ya huruma yoyote. Wanadamu wamekuwa hayawani hata kwa nduguzo kwani wamewafanya limbukeni wa kuwalamba miguu yao iliyojaa funza. Twawalamba hao watu hadi uparani na katu hawatupatii mkono wa buriani. Mema wanayowafanyia wananchi wenye dhiki ni kuwalaani kwa yoyote wanayoyafanya pasi hofu yoyote. Tumekuwa watumwa wao jambo ambalo limewapa kiburi cha jogoo la boma asiyekuwa na moyo wa kifalme wa nipe nikupe.
Hadhira yetu imekuwa milki yao ya kutusomba namna wanavyotaka huku pia shida zetu wanazipigia hesabu za tano ondoa sita! Kwa kweli misumari tuliyosulubiwa nayo ni wao wanasiasa walinunua kwa minajili ya kutugandamanisha katika dhiki zetu. Ehee! Maisha kizungumkuti! Imekuwa ajabu ya punda kujiwekelea mzigo halafu tena ahitaji abebwe kwa gari na huo huo mzigo wake. Tumekuwa viumbe wanaojitumbukiza kwa shimo tulionalo halafu baaye twahitaji mkono wa ibilisi utuokoe.
Kwangu maisha yamekuwa mazito hata kuyamiliki yamekuwa mzigo mwingine. Nimekuwa mpokezi wa misaada hadi wanaoileta wamechoka nami kwani nimekuwa kama mzigo kwao pia. Tangu utotoni nimekuwa nikiishi kambini kwa wakimbizi hata kwetu halisi sipajui wala siwezi kupafikiria kamwe. Kila uchao, wanasiasa hutupa sampuli ya vyakula kusomba akili zetu. Chakula hiki kama kawaida huwa hakina ladha wala shibe yoyote bali huwa ni cha kunifanya nisisahau ya kwamba kuna NGELI YA CHAKULA. Maishetu yamekuwa parakwanja ya matatizo yas’okuwa na kikomo.
Lililonibakia ni sala pekee kwa Rabuka mwenye kuumba na kutuneemesha kwa yoyote yale. Kichapo cha Mola ndicho kitakachotuokoa kwa hawa ndugu zetu wenye fitina na njaa ya makuu bila jasho. Humu duniani hakuna fimbo inayoweza kuwachapa kwani hata hizo fimbo ni wao ndio walizozipanda kwa mashamba yao ya miswada onevu. Kwa sasa nimebaki mnyonge lakini matumaini yangu ya kufika ng’ambo ile nyingine bado haijadidimia kamwe. Bado najipa moyo. Siasa ni unyevu ilhali wanasiasa ni mbao kwa hivyo siasa za wanasiasa ni KUNI MBICHI! La kunitia moyo sana ni ile tanuri nionayo ng’ambo ile! WAKENYA TUTAFIKA!

Comments

Popular posts from this blog

Does degree worth it?

Kisa cha Suleiman bwana Hamisi-kwa wapenzi wa Kiswahili pekee.